Rukia maudhui makuu
Pambazuko
Ukweli Hauna Kutu

Kimataifa

Dunia: Hapa na Pale

Mkenya adai ukosefu wa nguvu za kiume utambuliwe kisheria kama ulemavu, sarafu ya ukumbusho ya Trump yazinduliwa Marekani, Afrika yaidhinishiwa uwakilishi wa kudumu Umoja wa Mataifa, na Jenerali Muhoozi amtaja Rais Kagame kuwa mtu hatari.

Jumatatu, 7 Septemba 2026 · 06:00Dakika 2 kusomaToleo 181, uk. 4

Alia na nguvu za kiume.

MWANAUME mmoja Mkenya anataka matatizo kama vile ukosefu wa nguvu za kiume yatambuliwe kisheria kama ulemavu.

Katika ombi alilowasilisha bungeni, Dkt. Benson Kibore amesema tatizo la nguvu za kiume na ukosefu wa hamu ya kushiriki mapenzi, hali inayojulikana kama HSDD, linahitaji kushughulikiwa kupitia sheria na sera za afya.

Amesema matatizo hayo, ambayo hapo awali yalihusishwa zaidi na wazee, sasa yanaonekana pia miongoni mwa vijana.

Dkt. Kibore anarejelea utafiti wa 2026 uliofanywa Nairobi na kuchapishwa kwenye jarida la medRxiv, umeonyesha kuwa asilimia 10.4 ya vijana waliofanyiwa utafiti walikuwa na tatizo la nguvu za kiume. Wastani wa umri wao ulikuwa miaka 27.

Muhoozi: Kagame mtu hatari.

MKUU wa Majeshi ya Uganda, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, amezua mjadala mkali baada ya kuchapisha ujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa X unaomlenga Rais wa Rwanda, Paul Kagame, akimwelezea kuwa “Mtutsi hatari zaidi kuwahi kukutana naye maishani.”

Kauli hiyo imeibua tafsiri tofauti kuhusu uhusiano kati ya viongozi hao wawili, baadhi wakiitafsiri kama dokezo kwamba Rais Kagame ni mtu mwenye historia ya kutumia nguvu kali dhidi ya wapinzani wake.

Ujumbe huu wa Jenerali Muhoozi, ambaye pia ni mtoto wa Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, umeongeza maswali kuhusu uhusiano wa kisiasa na kiusalama kati ya Uganda na Rwanda.

Trump kwenye sarafu ya USD.

PICHA ya Rais wa Marekani, Donald Trump, imewekwa kwenye sarafu ya dola moja, ikiwa ni mara ya kwanza kwa picha ya rais aliye hai kuonekana kwenye fedha ya Marekani katika kipindi cha zaidi ya miaka 100.

Shirika la Uchapishaji wa Fedha la Marekani (U.S. Mint) limesema sarafu hiyo imetolewa kuadhimisha miaka 250 ya uhuru wa taifa hilo.

Jumatano iliyopita, Kampuni ya Marekani ya Mint ilizindua sarafu ya ukumbusho ya dola moja yenye picha ya Trump na kauli mbiu; “Tunamwamini Mungu”, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 250 ya Marekani.

Afrika ‘mpya’ yaidhinishwa UN.

BARAZA Kuu la Umoja wa Mataifa limeidhinisha kubadilishwa kwa ramani ya kawaida ya dunia na kuweka nyingine inayoonyesha ukubwa halisi wa bara la Afrika.

Hii iliyopo inarekebisha ramani ya Merchanter iliyotengenezwa 1569 ikionyesha Afrika ina ukubwa sawa na Greenland, wakati ukweli inaizidi mara 14.

Azimio hilo lenye lengo la “Kurekebisha Ramani,” liliwasilishwa na Togo na kuungwa mkono na nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU), lilipitishwa kwa uungwaji mkono wa mataifa 164, yakiwemo Ufaransa na Uingereza.

Marekani ndiyo nchi pekee iliyopiga kura ya kupinga, huku nchi sita zikijizuia kupiga kura.

Ingawa kura hiyo ya UN haina nguvu ya kisheria ya kulazimisha utekelezaji, itasababisha mabadiliko katika ramani zinazotumiwa na taasisi mbalimbali duniani kote.

  • Kimataifa

Soma Pia